Tuesday, August 27, 2013

Share:

KUPATA FAIDA KUBWA KWA UFUGAJI WA KUKU WA KIENYEJI KWA GHARAMA NDOGO




Unaweza kutunza kuku wa kienyeji na ukawa na kipato cha uhakika, pamoja na lishe nzuri kwa ajili ya familia.


 Ulishaji: Kuku wa kienyeji wanaweza kulishwa kwa kumia mahindi, mchele, na mabaki ya ugali. Vyakula hivi ni lazima vikaushwe vizuri na kusagwa vizuri. Ulishaji ni lazima ufanyike katika sehemu safi au kwa kutumia vyombo vilivyotengenezwa maalumu kwa ajilii ya kulishia kuku.

Banda: Kuku wawe wa kienyeji au wa kisasa, wanahitaji kuwa na banda zuri kwa ajili ya malazi na kuwalinda. Wanahitaji chumba chenye nafasi ya kutosha na kinachopitisha hewa ya kutosha. Ni lazima kuwawekea fito kwa kuwa ndege hupenda kupumzika juu ya fito. Ni lazima banda la kuku lifungwe vizuri nyakati za usiku ili kuzuia wanyama wanaoweza kuwadhuru kuku. Ni lazima liwe safi wakati wote ili kuzuia magonjwa kama vile mdondo na mengineyo. Usitumie pumba za mbao au nguo kuukuu kwenye viota vya kutagia kwani huchochea kuwepo utitiri na funza wa kuku. Inashauriwa kutumia mchanga laini.

Maji ya kunywa: Kuku wapatiwe maji safi. Ni lazima kuangalia mara kwa mara na kuyabadilisha maji. Kamwe usiwape kuku maji machafu.

Chanjo: Chanjo kwa mifugo ni lazima ili kuzuia mashambulizi ya magonjwa. Magonjwa yaliyozoeleka ni kama vile Mdondo, Kideri, Ndui ya kuku, na homa ya matumbo (typhoid). Chanjo kwa kawaida hutolewa mara moja kwa kila baada ya miezi miwili.

Uwekaji wa kumbukumbu: Kumbukumbu zijumuishe aina ya ulishaji, namba ya uzalishaji, muda wa mwisho wa matumizi, kiasi cha malisho kwa kila siku, idadi ya vifo, na idadi ya mayai yaliyozalishwa.

Mwanzoni unahitaji nini?

Wafugaji walio wengi wanauliza wanahitaji nini katika hatua za awali ili kuweza kuanzisha mradi wa ufugaji wa kuku. Hii itategemea aina ya kuku uliochagua kufuga.

Ni busara kuwa na vifaa muhimu vinavyohitajika na viwe katika hali ya usafi kabla ya kuweka kuku bandani mwako. Kama unaanza na vifaranga, vifuatavyo ni vifaa muhimu vinavyohitajika kwa ajili ya vifaranga 200.

• Tenga na utengeneze banda zuri lenye joto na hewa ya kutosha wakati wote.
• Vyombo vinne (4) vya kunyweshea maji, hii ni katika wiki 2 za mwanzo na uongeze vyombo taratibu kulingana na kuku wanavyokua.
• Vyombo vinne (4) vya kulishia chakula, na viongezeke kulingana na kuku wanavyokua.
• Matandazo makavu na safi, inaweza kuwa maranda au mabua ya ngano.
• Pakiti moja au mbili za dawa ya Coccid (hii inapatikana katika maduka yote ya kilimo). Hata hivyo, utaratibu wa chanjo ni lazima ukamilishwe.
• Chakula kwa ajili ya vifaranga ambacho kimezalishwa na watengenezaji wanaoaminika.

Ufugaji wa kuku unaweza kuongeza kipato cha familia


 “Mimi ni mfugaji mdogo wa kuku wa kienyeji katika viunga vya jiji la Dar es Salaam. Nina kuku 65 ambao ninawafuga katika eneo dogo nyumbani. Nilivutiwa kuanza ufugaji wa kuku wa kienyeji baada ya kutumia fedha nyingi kununua mayai ya kuku wa kienyeji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Nilikua natumia zaidi ya shilingi elfu thelathini (30000) kila mwezi kwa ajili ya kununua mayai ya kuku. Ndivyo anavyoanza kusimulia mafanikio yake Bi. Haika Mcharo, ambae ni mfugaji.

Msukumo huu ndio ulinifanya niwe na wazo la kufuga kuku wa kienyeji. Nilianza na kuku 12 na sasa ninao kuku 65 wanaotaga na wanaotarajia kutaga. Sipati faida kubwa sana ila kwa sasa sinunui tena mayai bali ninauza mayai. Faida nyingine ni upatikanaji wa mbolea unaotokana na kinyesi cha kuku. Ninatumia kwa kulimia bustani ya maua na mboga mboga, pia majirani wenye uhitaji wanakuja kwangu kubeba. Kwangu, kufuga kuku wa kienyeji kuna umuhimu sana kwani najiongezea kipato, ni kama akiba ambapo faida yake huzaana tu kama riba ya benki.

 Malengo yangu ni kuwa na kuku wengi ambao watagharamia karo ya watoto wangu, malipo ya hospitali na gharama nyingine za nyumbani. Sihangaiki sana katika kupata chakula cha kuku ninaowafuga kwani mbali na mchanganyiko wa chakula ninaowanunulia kwa jina maarufu layers mash pia huwapa mabaki ya chakula, majani, mabaki kutoka jikoni na, vyakula vya kujitafutia muda wa jioni napowafungulia. Mfumo huu wa kufuga kuku kwa njia ya kienyeji unatumia viungo vinavyopatikana kwa urahisi. Huwa ninazingatia tiba mara ninapoona kuku wangu wanadhoofika. Nina daktari maalumu wa mifugo ambaye hunipa ushauri wa tiba ipi niitumie na kwa wakati gani. Pia ninazingatia chanjo zote ili kuwalinda na magonjwa.

Hakuna changamoto kubwa ninayokumbana nayo bali hali ya kuwatunza na kuwalisha inahitaji umakini mkubwa ili wakue na kupata kile ninachokitarajia. Ufugaji wa kuku wa kienyeji ni rahisi na hauhitaji gharama kubwa kwani waweza ukafuga kama kikundi au mtu mmoja mmoja. Nimefanikiwa kuwashawishi akina mama 5 ambao kwa sasa wameanza ufugaji wa kuku wa kienyeji. Lengo ni kuwa na kikundi ambacho tunaweza kupata soko la kuuza mayai kwa uhakika na upatikanaji wake uwe wa uhakika

source;mkulima mbunifu
Share:

MIPANGO MIZURI HULETA MAFANIKIO KATIKA UFUGAJI WA NGOMBE WA MAZIWA




Mipango thabiti huleta mafanikio katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa. Wafugaji waliofanikiwa wanafahamu fika kuwa katika uzalishaji wa maziwa 20% inatokana na aina ya ng’ombe na 80% matunzo.
Watu wengi ambao wanataka kuanzisha ufugaji wa ng’ombe, lakini hawajui ni wapi pa kuanzia. Kwa kawaida, wao wanaweka pesa, kutafuta ng’ombe, kununua na mwisho hupata ng’ombe. Hapo ndipo kuhangaika na kupata msongo wa mawazo kwa mfugaji huanza kwa kuwa ng’ombe hazalishi maziwa kutokana na aina yake pekee.

Kwa wafugaji wadogo walio wengi, wakati ambapo ng’ombe anafika zizini kwake wanakuwa bado hawajawa tayari kumpokea ng’ombe huyo kwa ajili ya ufugaji. Ili ujasiria mali kwa njia ya ng’ombe uweze kufanikiwa na kumfaidisha mfugaji kiuchumi, mfugaji ni lazima ahakikishe kuwa miundo mbinu muhimu inakuwa tayari kabla ya kumleta ng’ombe.


Kwa mujibu wa mwongozi wa kitabu cha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa Afrika ya mashariki, ng’ombe wa maziwa ni lazima wapate mahitaji yafuatayo:
• Malisho bora na maji safi ya kunywa
• Afya bora bila majeraha
• Mazingira safi ikiwa ni pamoja na  banda lililojengwa vizuri
• Uangalizi mzuri na wa kirafiki,  ambao humfanya ng’ombe kuwa mtulivu bila kuwa na msongo.

Bila mahitaji haya muhimu, na mfugaji kutokumtunza ng’ombe vizuri, asitegemee kuwa ng’ombe huyo atazalisha kiwango kizuri cha maziwa. Uzalishaji wa kiwango cha maziwa na ubora wake unategemeana kwa kiasi kikubwa na mambo hayo yaliyotajwa hapo juu. Wataalamu wanasema kuwa 20% ya uzalishaji wa ng’ombe inatokana na aina ya ng’ombe na 80% matunzo kutoka kwa mfugaji. Muhudumie ng’ombe wako vizuri naye atarudisha kwa kuzalisha maziwa vizuri.

Mipango

Wafugaji ni lazima wawe na mipango thabiti kwa ajili ya ufugaji wa ng’ombe. Hii hujumuisha idadi ya ng’ombe mfugaji anayotaka kufuga, pamoja na kufahamu ni kiasi gani cha malisho kinachohitajika kwa kipindi chote cha mwaka. Mfugaji pia anapaswa kufahamu kuwa ni kwa namna gani malisho yanafaa kutolewa kwa wanyama.

Mfugaji ni lazima pia apange ni kwa namna gani atapata malisho kwa kipindi chote. Hii inamaanisha kuwa ni muda gani atapanda, kuvuna na kuhifadhi. Mipango ni nguzo muhimu sana kwa kuwa inawezesha kusaidia kufahamu ni nini cha kufanya, namna ya kufikia malengo yaliyokusudiwa, na ni hatua gani imefikiwa. Mfugaji ambaye hana mipango thabiti ni sawa na mtu anayeanza safari bila kufahamu mwisho wa safari yake ni wapi.

Mahitaji ya mlo kamili

Shughuli ya ufugaji wako itakamalika siku ambayo utaweza kuelewa uhusiano kati ya ulishaji wa ng’ombe, uzalishaji wa maziwa na mapato. Endapo ng’ombe wa maziwa atalishwa kwa malisho hafifu ni dhahiri kuwa uzalishaji wa maziwa pia utakuwa hafifu.

Malisho bora

Tafuta ni aina gani ya malisho hufanya vizuri katika ukanda wako. Malisho endelevu hutegemeana kwa kiasi kikubwa na aina ya malisho na utunzaji wake shambani mwako. Chukulia kuwa wewe ni mfugaji mdogo na hauwezi kumudu gharama za umwagiliaji, ni lazima utumie kwa kiasi kikubwa malisho ya wakati wa mvua na kuhifadhi ili kuweza kuyatumia wakati wa kiangazi.

Inashauriwa kupanda majani ya malisho kwa kiasi kikubwa uwezavyo wakati wa mvua. Wahamasishe majirani zako kupanda malisho pia, ili baadaye uweze kununua kutoka kwao. Matete, nyasi, majani ya mtama, majani ya mahindi, lusina, desmodiamu, na alizeti ni miongoni mwa malisho ambayo hufanya vizuri katika maeneo mengi nchini Tanzania.

Kiwango cha kutosha

Fahamu ni kiwango gani kinachotosha kwa kila ng’ombe wako. Hii itakusaidia kufahamu ni kiasi gani cha malisho upande na ni kiasi gani uhifadhi. Kwa wastani, ngombe wa maziwa aliyekomaa mwenye uzito wa kilo 400, anayefugwa ndani ana uwezo wa kula kilo 12 za majani makavu kwa siku. Kumbuka kuwa endapo mifugo yako haitapata malisho ya kutosha wataonesha kwa muonekana wao, na kisha kukupa adhabu kwa kuzalisha maziwa kidogo sana. Kama kanuni inavyoeleza, hakikisha kuwa 15%-18% ya malisho yote ni protini.

Zingatia utunzaji na uzalishaji wa malisho vizuri

Wafugaji walio wengi hukwepa kupanda majani ya malisho kwa kuogopa gharama ya mbolea na mbegu. Kwa uzoefu wetu mfugaji anaweza kutumia mbolea inayotokana na wanyama kupanda malisho na kuyatunza vizuri. Matete ni moja wapo ya malisho hayo. Endapo malisho hayo yatawekwa mbolea vizuri, shamba dogo tu la malisho linaweza kukupatia malisho ya mifugo kwa kipindi chote cha mwaka.

Weka malisho katika hali ya usafi

Hifadhi malisho katika sehemu nzuri, sehemu ambayo hayatapigwa na jua moja kwa moja, mvua au kuwepo uwezekano wa vitu vingine vinavyoweza kuyaharibu kama vile siafu na wadudu wengineo. Majani ya malisho ni lazima yanyaushwe vizuri kuepuka viini vya sumu vinavyoweza kuwepo kwenye malisho. Mfugaji anaweza kuamua juu ya ubora wa malisho kutokana na muonekano wake, harufu na mguso. Malisho mabichi yenye wingi wa majani kuliko shina, yenye kijani kilichokolea, na ambayo yana mguso nyororo, ni moja ya malisho bora ukilinganisha na yale yenye ugumu, shina kubwa na rangi ya njano. Epuka kulisha mifugo yako kwa kutumia malisho yenye ukungu kwa kuwa yanaweza kuwa na sumu.

Kuweka kumbukumbu ni muhimu

Uwekaji wa kumbukumbu ni muhimu lakini huwa hauzingatiwi na wafugaji walio wengi. Baadhi ya wafugaji huona kama uwekaji wa kumbukumbu ni kazi ya ziada, ambayo kulingana na wao haina uhusiano wowote na mapato yanayotokana na shughuli zao. Hata hivyo, bila uwekaji sahihi wa kumbukumbu, mfugaji hawezi kufahamu ni mapato kiasi gani anayopata kutokana na shughuli ya ufugaji. Ni kwa namna gani mfugaji anaweza kufahamu wakati wa kumpandisha ng’ombe wake, kama hajui kuwa zimepita siku ngapi tangu ng’ombe huyo alipozaa!

Source: mkulima mbunifu
Share:

KUHUSU MMILIKI WA BLOG HII

My photo
Naitwa faraja Mmasa a.k.a Moa,Mkazi na mzaliwa wa Wilaya ya Gairo Morogoro.KARIBU KATIKA BLOG hii tuelimishane mambo mbalimbali.Inatupasa kuwa na ufahamu wa mambo mbalimbali ili tuweze kuyatawala Mazingira yetu .Kuwa na Mwanasheria au Mhasibu haimanishi unatikiwa kujua au kufuatilia maswala ya uhasibu na sheria tu.Mfano nyumba yako au ndoa yako hutaindesha kwa taaluma uliyonayo.Vile vile huwezi kuendesha ujasiliamali kwa mafanikio kwa shahada yako ya uhandisi.TUNAANGAMIA KWA KUKOSA MAARIFA

UJUMBE WA LEO

MIUJIZA MINGI INAYOTOKEA KATIKA MAISHA IPO KATIKA MAWAZO,FIKRA,NA IMANI ALIYONAYO MWANADAMU HUSIKA

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

GAR AD2

GAR AD2

GARI ADVERT

GARI ADVERT

Castrol

Castrol
Powered by Blogger.