Tuesday, August 27, 2013
KUPATA FAIDA KUBWA KWA UFUGAJI WA KUKU WA KIENYEJI KWA GHARAMA NDOGO
Unaweza
kutunza kuku wa kienyeji na ukawa na kipato cha uhakika, pamoja na lishe nzuri
kwa ajili ya familia.
Ulishaji: Kuku wa kienyeji wanaweza kulishwa
kwa kumia mahindi, mchele, na mabaki ya ugali. Vyakula hivi ni lazima vikaushwe
vizuri na kusagwa vizuri. Ulishaji ni lazima ufanyike katika sehemu safi au kwa
kutumia vyombo vilivyotengenezwa maalumu kwa ajilii ya kulishia kuku.
Banda: Kuku
wawe wa kienyeji au wa kisasa, wanahitaji kuwa na banda zuri kwa ajili ya
malazi na kuwalinda. Wanahitaji chumba chenye nafasi ya kutosha na
kinachopitisha hewa ya kutosha. Ni lazima kuwawekea fito kwa kuwa ndege hupenda
kupumzika juu ya fito. Ni lazima banda la kuku lifungwe vizuri nyakati za usiku
ili kuzuia wanyama wanaoweza kuwadhuru kuku. Ni lazima liwe safi wakati wote
ili kuzuia magonjwa kama vile mdondo na mengineyo. Usitumie pumba za mbao au
nguo kuukuu kwenye viota vya kutagia kwani huchochea kuwepo utitiri na funza wa
kuku. Inashauriwa kutumia mchanga laini.
Maji ya
kunywa: Kuku wapatiwe maji safi. Ni lazima kuangalia mara kwa mara na
kuyabadilisha maji. Kamwe usiwape kuku maji machafu.
Chanjo:
Chanjo kwa mifugo ni lazima ili kuzuia mashambulizi ya magonjwa. Magonjwa
yaliyozoeleka ni kama vile Mdondo, Kideri, Ndui ya kuku, na homa ya matumbo
(typhoid). Chanjo kwa kawaida hutolewa mara moja kwa kila baada ya miezi
miwili.
Uwekaji wa
kumbukumbu: Kumbukumbu zijumuishe aina ya ulishaji, namba ya uzalishaji, muda
wa mwisho wa matumizi, kiasi cha malisho kwa kila siku, idadi ya vifo, na idadi
ya mayai yaliyozalishwa.
Mwanzoni
unahitaji nini?
Wafugaji
walio wengi wanauliza wanahitaji nini katika hatua za awali ili kuweza
kuanzisha mradi wa ufugaji wa kuku. Hii itategemea aina ya kuku uliochagua
kufuga.
Ni busara
kuwa na vifaa muhimu vinavyohitajika na viwe katika hali ya usafi kabla ya
kuweka kuku bandani mwako. Kama unaanza na vifaranga, vifuatavyo ni vifaa
muhimu vinavyohitajika kwa ajili ya vifaranga 200.
• Tenga na
utengeneze banda zuri lenye joto na hewa ya kutosha wakati wote.
• Vyombo
vinne (4) vya kunyweshea maji, hii ni katika wiki 2 za mwanzo na uongeze vyombo
taratibu kulingana na kuku wanavyokua.
• Vyombo
vinne (4) vya kulishia chakula, na viongezeke kulingana na kuku wanavyokua.
• Matandazo
makavu na safi, inaweza kuwa maranda au mabua ya ngano.
• Pakiti
moja au mbili za dawa ya Coccid (hii inapatikana katika maduka yote ya kilimo).
Hata hivyo, utaratibu wa chanjo ni lazima ukamilishwe.
• Chakula
kwa ajili ya vifaranga ambacho kimezalishwa na watengenezaji wanaoaminika.
Ufugaji wa
kuku unaweza kuongeza kipato cha familia
“Mimi ni mfugaji mdogo wa kuku wa kienyeji
katika viunga vya jiji la Dar es Salaam. Nina kuku 65 ambao ninawafuga katika
eneo dogo nyumbani. Nilivutiwa kuanza ufugaji wa kuku wa kienyeji baada ya
kutumia fedha nyingi kununua mayai ya kuku wa kienyeji kwa ajili ya matumizi ya
nyumbani.
Nilikua
natumia zaidi ya shilingi elfu thelathini (30000) kila mwezi kwa ajili ya
kununua mayai ya kuku. Ndivyo anavyoanza kusimulia mafanikio yake Bi. Haika
Mcharo, ambae ni mfugaji.
Msukumo huu
ndio ulinifanya niwe na wazo la kufuga kuku wa kienyeji. Nilianza na kuku 12 na
sasa ninao kuku 65 wanaotaga na wanaotarajia kutaga. Sipati faida kubwa sana
ila kwa sasa sinunui tena mayai bali ninauza mayai. Faida nyingine ni upatikanaji
wa mbolea unaotokana na kinyesi cha kuku. Ninatumia kwa kulimia bustani ya maua
na mboga mboga, pia majirani wenye uhitaji wanakuja kwangu kubeba. Kwangu,
kufuga kuku wa kienyeji kuna umuhimu sana kwani najiongezea kipato, ni kama
akiba ambapo faida yake huzaana tu kama riba ya benki.
Malengo yangu ni kuwa na kuku wengi ambao
watagharamia karo ya watoto wangu, malipo ya hospitali na gharama nyingine za
nyumbani. Sihangaiki sana katika kupata chakula cha kuku ninaowafuga kwani
mbali na mchanganyiko wa chakula ninaowanunulia kwa jina maarufu layers mash
pia huwapa mabaki ya chakula, majani, mabaki kutoka jikoni na, vyakula vya
kujitafutia muda wa jioni napowafungulia. Mfumo huu wa kufuga kuku kwa njia ya
kienyeji unatumia viungo vinavyopatikana kwa urahisi. Huwa ninazingatia tiba
mara ninapoona kuku wangu wanadhoofika. Nina daktari maalumu wa mifugo ambaye
hunipa ushauri wa tiba ipi niitumie na kwa wakati gani. Pia ninazingatia chanjo
zote ili kuwalinda na magonjwa.
Hakuna
changamoto kubwa ninayokumbana nayo bali hali ya kuwatunza na kuwalisha
inahitaji umakini mkubwa ili wakue na kupata kile ninachokitarajia. Ufugaji wa
kuku wa kienyeji ni rahisi na hauhitaji gharama kubwa kwani waweza ukafuga kama
kikundi au mtu mmoja mmoja. Nimefanikiwa kuwashawishi akina mama 5 ambao kwa
sasa wameanza ufugaji wa kuku wa kienyeji. Lengo ni kuwa na kikundi ambacho
tunaweza kupata soko la kuuza mayai kwa uhakika na upatikanaji wake uwe wa
uhakika
source;mkulima mbunifu
MIPANGO MIZURI HULETA MAFANIKIO KATIKA UFUGAJI WA NGOMBE WA MAZIWA
Mipango
thabiti huleta mafanikio katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa. Wafugaji
waliofanikiwa wanafahamu fika kuwa katika uzalishaji wa maziwa 20% inatokana na
aina ya ng’ombe na 80% matunzo.
Watu wengi
ambao wanataka kuanzisha ufugaji wa ng’ombe, lakini hawajui ni wapi pa kuanzia.
Kwa kawaida, wao wanaweka pesa, kutafuta ng’ombe, kununua na mwisho hupata
ng’ombe. Hapo ndipo kuhangaika na kupata msongo wa mawazo kwa mfugaji huanza
kwa kuwa ng’ombe hazalishi maziwa kutokana na aina yake pekee.
Kwa wafugaji
wadogo walio wengi, wakati ambapo ng’ombe anafika zizini kwake wanakuwa bado
hawajawa tayari kumpokea ng’ombe huyo kwa ajili ya ufugaji. Ili ujasiria mali
kwa njia ya ng’ombe uweze kufanikiwa na kumfaidisha mfugaji kiuchumi, mfugaji
ni lazima ahakikishe kuwa miundo mbinu muhimu inakuwa tayari kabla ya kumleta
ng’ombe.
Kwa mujibu
wa mwongozi wa kitabu cha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa Afrika ya mashariki,
ng’ombe wa maziwa ni lazima wapate mahitaji yafuatayo:
• Malisho
bora na maji safi ya kunywa
• Afya bora
bila majeraha
• Mazingira
safi ikiwa ni pamoja na banda
lililojengwa vizuri
• Uangalizi
mzuri na wa kirafiki, ambao humfanya
ng’ombe kuwa mtulivu bila kuwa na msongo.
Bila
mahitaji haya muhimu, na mfugaji kutokumtunza ng’ombe vizuri, asitegemee kuwa
ng’ombe huyo atazalisha kiwango kizuri cha maziwa. Uzalishaji wa kiwango cha
maziwa na ubora wake unategemeana kwa kiasi kikubwa na mambo hayo yaliyotajwa
hapo juu. Wataalamu wanasema kuwa 20% ya uzalishaji wa ng’ombe inatokana na
aina ya ng’ombe na 80% matunzo kutoka kwa mfugaji. Muhudumie ng’ombe wako
vizuri naye atarudisha kwa kuzalisha maziwa vizuri.
Mipango
Wafugaji ni
lazima wawe na mipango thabiti kwa ajili ya ufugaji wa ng’ombe. Hii hujumuisha
idadi ya ng’ombe mfugaji anayotaka kufuga, pamoja na kufahamu ni kiasi gani cha
malisho kinachohitajika kwa kipindi chote cha mwaka. Mfugaji pia anapaswa
kufahamu kuwa ni kwa namna gani malisho yanafaa kutolewa kwa wanyama.
Mfugaji ni
lazima pia apange ni kwa namna gani atapata malisho kwa kipindi chote. Hii
inamaanisha kuwa ni muda gani atapanda, kuvuna na kuhifadhi. Mipango ni nguzo
muhimu sana kwa kuwa inawezesha kusaidia kufahamu ni nini cha kufanya, namna ya
kufikia malengo yaliyokusudiwa, na ni hatua gani imefikiwa. Mfugaji ambaye hana
mipango thabiti ni sawa na mtu anayeanza safari bila kufahamu mwisho wa safari
yake ni wapi.
Mahitaji ya
mlo kamili
Shughuli ya
ufugaji wako itakamalika siku ambayo utaweza kuelewa uhusiano kati ya ulishaji
wa ng’ombe, uzalishaji wa maziwa na mapato. Endapo ng’ombe wa maziwa atalishwa
kwa malisho hafifu ni dhahiri kuwa uzalishaji wa maziwa pia utakuwa hafifu.
Malisho bora
Tafuta ni
aina gani ya malisho hufanya vizuri katika ukanda wako. Malisho endelevu
hutegemeana kwa kiasi kikubwa na aina ya malisho na utunzaji wake shambani
mwako. Chukulia kuwa wewe ni mfugaji mdogo na hauwezi kumudu gharama za
umwagiliaji, ni lazima utumie kwa kiasi kikubwa malisho ya wakati wa mvua na
kuhifadhi ili kuweza kuyatumia wakati wa kiangazi.
Inashauriwa
kupanda majani ya malisho kwa kiasi kikubwa uwezavyo wakati wa mvua.
Wahamasishe majirani zako kupanda malisho pia, ili baadaye uweze kununua kutoka
kwao. Matete, nyasi, majani ya mtama, majani ya mahindi, lusina, desmodiamu, na
alizeti ni miongoni mwa malisho ambayo hufanya vizuri katika maeneo mengi
nchini Tanzania.
Kiwango cha
kutosha
Fahamu ni
kiwango gani kinachotosha kwa kila ng’ombe wako. Hii itakusaidia kufahamu ni
kiasi gani cha malisho upande na ni kiasi gani uhifadhi. Kwa wastani, ngombe wa
maziwa aliyekomaa mwenye uzito wa kilo 400, anayefugwa ndani ana uwezo wa kula
kilo 12 za majani makavu kwa siku. Kumbuka kuwa endapo mifugo yako haitapata
malisho ya kutosha wataonesha kwa muonekana wao, na kisha kukupa adhabu kwa
kuzalisha maziwa kidogo sana. Kama kanuni inavyoeleza, hakikisha kuwa 15%-18%
ya malisho yote ni protini.
Zingatia
utunzaji na uzalishaji wa malisho vizuri
Wafugaji
walio wengi hukwepa kupanda majani ya malisho kwa kuogopa gharama ya mbolea na
mbegu. Kwa uzoefu wetu mfugaji anaweza kutumia mbolea inayotokana na wanyama
kupanda malisho na kuyatunza vizuri. Matete ni moja wapo ya malisho hayo.
Endapo malisho hayo yatawekwa mbolea vizuri, shamba dogo tu la malisho linaweza
kukupatia malisho ya mifugo kwa kipindi chote cha mwaka.
Weka malisho
katika hali ya usafi
Hifadhi
malisho katika sehemu nzuri, sehemu ambayo hayatapigwa na jua moja kwa moja,
mvua au kuwepo uwezekano wa vitu vingine vinavyoweza kuyaharibu kama vile siafu
na wadudu wengineo. Majani ya malisho ni lazima yanyaushwe vizuri kuepuka viini
vya sumu vinavyoweza kuwepo kwenye malisho. Mfugaji anaweza kuamua juu ya ubora
wa malisho kutokana na muonekano wake, harufu na mguso. Malisho mabichi yenye
wingi wa majani kuliko shina, yenye kijani kilichokolea, na ambayo yana mguso
nyororo, ni moja ya malisho bora ukilinganisha na yale yenye ugumu, shina kubwa
na rangi ya njano. Epuka kulisha mifugo yako kwa kutumia malisho yenye ukungu
kwa kuwa yanaweza kuwa na sumu.
Kuweka
kumbukumbu ni muhimu
Uwekaji wa
kumbukumbu ni muhimu lakini huwa hauzingatiwi na wafugaji walio wengi. Baadhi
ya wafugaji huona kama uwekaji wa kumbukumbu ni kazi ya ziada, ambayo kulingana
na wao haina uhusiano wowote na mapato yanayotokana na shughuli zao. Hata
hivyo, bila uwekaji sahihi wa kumbukumbu, mfugaji hawezi kufahamu ni mapato
kiasi gani anayopata kutokana na shughuli ya ufugaji. Ni kwa namna gani mfugaji
anaweza kufahamu wakati wa kumpandisha ng’ombe wake, kama hajui kuwa zimepita
siku ngapi tangu ng’ombe huyo alipozaa!
Source: mkulima mbunifu