Unaweza kulima kabichi msimu wote wa
mwaka. Soko lake ni la uhakika katika kipindi chote na ni muhimu kwa
afya. Pia, linaweza kutumika kama malisho ya mifugo
Kabichi ni moja ya mazao yaliyomo katika
jamii ya mimea inayojumuisha mimea ya kaulifulawa (cauliflower ),
kabichi ya kichina na kale. Kwa kawaida kabichi hupandwa kwa msimu
mmoja, lakini iwapo itakuzwa kwa ajili ya kutoa mbegu hukuzwa zaidi ya
msimu mmoja. Endapo inalimwa sehemu yenye maji ya kutosha, inaweza
kulimwa msimu wote wa mwaka. Kichwa cha kabichi kinapofunga vizuri,
hutumika kama chakula na huvunwa baada ya kufunga na kukomaa vizuri.
Mizizi: Mizizi ya kabichi
hutawanyika ardhini vizuri. Kwa kawaida, huenda chini kiasi cha
sentimita ishirini (20 sm), na hujitawanya kwa kiasi cha sentimita
sabini na tano (75sm).
Shina: Shina la mmea wa kabichi huwa na rangi ya kijani au zambarau. Hii hutegemeana na aina ya kabichi, na kwa kawaida ni fupi.
Hali ya hewa: Kabichi hustawi vyema katika sehemu yenye hali ya baridi, hali ya joto jingi haifai kwa kabichi kwa kuwa huathiri uotaji na ukuaji wake. Joto jingi pia husababisha kulegea kwa vichwa vilivyofunga. Zao hili hustawi vema katika maeneo yenye mwinuko wa zaidi ya mita 100 toka usawa wa bahari.
Udongo: Zao hili linaweza kustawishwa kwenye udongo wa aina yoyote mradi tu udongo huo usiwe na chumvichumvi nyingi na usiotuhamisha maji. Udongo wa kichanga na ule usio na rutuba ya kutosha husababisha kabichi kukomaa upesi na kuzaa kabichi hafifu zenye vichwa vidogo.
Kitalu: Kitalu ni muhimu katika
uzalishji wa zao hili. Ni vema kutengeneza matuta yenye upana wa mita
moja, na urefu wowote kulingana na matakwa ya mkulima. Mbolea za samadi
na zenye asili ya chokaa zichanganywe vizuri kwenye udongo. Kiasi cha
gramu 500 za mbegu huhitajika kwa hekta moja. Katika upandaji kwenye
kitalu ni vizuri kutengeneza mistari katika tuta, umbali toka mstari
hadi mstari uwe sentimita ishirini (20). Udongo kiasi kidogo utumike
katika kufunika mbegu.
Baada ya mbegu kuota ni vizuri kupunguza
baadhi ya miche na uwe katika kipimo cha sentimita 2-3 toka mche hadi
mche. Hii itasaidia kuwa na miche mifupi na yenye nguvu. Inafaa
kunyeshea kitalu mara moja au mbili kwa siku na katika sehemu za joto ni
vizuri kuweka kivuli katika matuta. Katika wiki ya tatu, hadi wiki ya
nne, ni vyema kuondoa kivuli kidogo kidogo huku ukipunguza unyeshaji.
Hali hii itasaidia miche isipate mshtuko wa uhamishaji shambani.